Habari
WATAALAM WA WIZARA ZA UJENZI NA UCHUKUZI TANZANIA BARA NA ZANZIBAR KUIMARISHA USHIKIRIANO KIUTENDAJI

Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar kupitia Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi Tanzania na Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano zimekubaliana kukutana kila baada ya miezi mitatu ili kujadili na kutafuta suluhu ya changamoto mbalimbali zinazokabili wizara hizo.
Akizungumza mjini Unguja wakati wa kikao kilichojumuisha Viongozi na Wataalam wa Wizara hizo, Katibu Mkuu wa wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Serikali ya Mapinduzi Zanzibar Hadija Hamisi Rajabu amesema mafanikio yoyote yanatokea kwa kupanga na kutekeleza mikakati ya kutatua changamoto kwa pamoja baina ya Serikali hizo.
“Wananchi wanatutegemea sana hasa kwenye upatikanaji wa huduma bora na zenye viwango na sisi ndio watendaji katika maeneo yote hasa ukizungatia kuwa sisi tuawajengea miundombinu, hivyo kupitia vikao hivi nina uhakika tutafika tutafika mbali sana kwenye utendaji wetu’ amesema Katibu Mkuu Hadija.
Katibu Mkuu Hadija amesema pamoja Serikali hizo kuwa na taasisi zinazojitegemea kwenye maeneo mbalimbali zinazohusika na miundombinu msisitizo uliowekwa kwenye taasisi za Muungano utawekwa pia kwenye taasisi zisizo za Muungano ili kuongeza ufanisi na utendaji kuwa wenye tija.
Kwa upande wake Naibu katibu Mkuu kutoka Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi Tanzania, Dkt. Ally Possi amesema kuwa uwepo wa vikao hivyo utaongeza chachu na kasi ya kuwapatia Watanzania na Wazanzibar maendeleo ambayo wanayataka na kwa wakati.
Dkt. Possi ameongeza kuwa vikao hivyo vitakuwa vikifanyika kuanzia ngazi ya wataalam, ngazi na Makatibu Wakuu na ngazi ya Mawaziri ili kuhakikisha kuwa maamuzi yanayofanyika kwenye maazimio yanakuwa na matokeo chanya kwa viongozi na wananchi kwa ujuma.
Wataalam Wizara hizo wamekutana kisiwani Unguja kwa siku mbili lengo likiwa ni kujadili na kuangalia namna bora ya kushirikiana katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo nchini hasa kwenye eneo Miundombinu.