Tanzania emblem
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Wizara ya Ujenzi

Habari

WATAALAM SMZ NA SJMT WABADILISHANA UZOEFU SEKTA YA UJENZI: DKT. MSONDE


Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Ujenzi Dkt. Charles Msonde amesema ushirikiano baina ya Wizara ya Ujenzi (SJMT) na Wizara ya Ujenzi, Mawasiliano na Uchukuzi (SMZ) umepelekea kubadilishana ujuzi na uzoefu kwa wataalam katika sekta hiyo kwa upande wa Tanzania Bara na Visiwani, ili ujuzi unaofahamika Bara uje ufahamike na Zanzibar pia.

Dkt. Msonde ameyasema hayo alipokuwa akifunga Mkutano wa Saba wa Ushirikiano Baina ya Wizara ya Ujenzi (SJMT) na Wizara ya Ujenzi, Mawasiliano na Uchukuzi (SMZ) uliofanyika katika ukumbi wa ZURA -Maisara Visiwani Zanzibar tarehe 02 Disemba,2024.

"Kwa mfano hapa Zanzibar tumeshuhudia teknolojia mpya ya ujenzi wa miundombinu ya barabara, wataalamu wetu wameenda kuangalia na kujifunza mambo mengi yanayofanyika hapa, ili kwa namna gani yaweze kufanyika kule Bara" amesema Dkt.Msonde.

Amesema changamoto za ujenzi wa miundombinu zilizopo Tanzania Bara na Visiwani vivyo hivyo zipo, kwahiyo wamekaa na kujadiliana kwa pamoja wafanyeje ili kupata ufumbuzi wa changamoto hizo kwa upande wa Bara na Visiwani.

Dkt.Msonde amesema kikao hicho kimekuwa na mafanikio makubwa sana, na wataalamu kutoka Bara wamejifunza mambo mengi ya utekelezaji wa miradi, hivyo amempongeza Rais wa Zanzibar Dkt. Hussein Ali Mwinyi kwa kazi kubwa anayoifanya katika kusimamia miundombinu ya ujenzi Zanzibar.

"Hali ya Zanzibar imefunguka sana, na haya ndio yanayofanywa Tanzania Bara pia na Rais Dkt.Samia Suluhu Hassan, ukienda kule Tanzania Bara utaona kila kona barabara zinatengenezwa, kila kona majengo yanajengwa" alisema Dkt.Msonde.

Aidha, Dkt.Msonde amesema mambo waliyoyapata na kujifunza katika kikao hicho wataenda kuwashauri viongozi (Mawaziri) wote wa pande mbili Zanzibar na Tanzania Bara ili kuleta ustawi wa miundombinu ya ujenzi Tanzania Bara na Visiwani.

Kwa upande wake Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi, Mawasiliano na Uchukuzi (SMZ) Dkt.Habiba Hassan Omar amesema kikao hicho kitawasaidia wao na wataalamu wao ili kuweza kubadilishana uzoefu katika kutengeneza miundombinu, kuishughulikia miundombinu na kujenga uwezo wa wataalamu.

"Kikao hichi ni kikao cha kupangwa na tumepanga kila mwaka tunatakiwa tufanye zaidi ya mara moja ili tuweze kukutana na kubadilishana uzoefu wa teknolojia ambao Bara wanautumia na sisi huku Zanzibar tunautumia" alisema Dkt.Habiba.