Tanzania emblem
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Wizara ya Ujenzi

Habari

WAFANYABIASHARA WARUHUSIWA KUTUMIA BANDARI YA UJIJI


Serikali kupitia Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA) imetoa kibali kwa wafanyabiashara wanaofanya ya shughuli za usafiri na usafirishaji wa mizigo na abiria kupitia bandari ya Ujiji mkoani Kigoma kutumia sehemu ya miundombinu iliyokamilika kwa sasa ili kupunguza gharama kubwa wanazotumia kwa kutumia eneo eneo la nje ya bandari hiyo.

 

Akizungumza wakati alipotembelea bandari hiyo mkoani humo Naibu Waziri wa Uchukuzi Atupele Mwakibete amesema matumizi ya miundombinu hiyo iliyokamilika kwa sasa yataongeza usalama kwa abiria na mizigo inayosafirisha na kuingia bandarini hapo kutoka maeneo mengine ndani na nchi Jirani zinazozunguka Mkoa huo.

 

“Wakati TPA inaendelea kukamilisha sehemu ya mradi iliyobaki ya bandari hii basi miundombinu iliyokamilika kwa sasa ianze kutumika ili kupunguza changamoto ambazo zinajitokeza kwa sasa ambapo wafanyabiashara hao hulamika kushushia abiria na mizigo kwenye mazingira yasiyo salama’ amesisitiza Naibu Waziri Mwakibete.

 

Naibu Waziri Mwakibete amewataka TPA kufanya maamuzi sahihi ndani ya wiki mbili kuhusu uendelezaji wa bandari hiyo ambayo ujenzi wake umekuwa ukisusa sua kwa sababu ya changamoto ya kina cha maji kupanda na kushuka.

 

Naye Mkuu wa Wilaya wa Kigoma Ester Mahawe ameishukuru Serikali ya awamu ya sita kwa kusikiliza kilio cha wakazi hao ambacho kimekuwepo kwa muda mrefu na kusema Mkoa utaendelea kutoa ushirikiano kwa mkandarasi ili akamilishe sehemu ya mradi iliyobaki.

 

Kaimu Meneja Bandari za Ziwa Tanganyika, Edward Mabula amesema TPA iko hatua za mwisho za kupitia taarifa ya tume ya wataalam iliyowasilisha kuhusu changamoto za bandari hiyo na  amemuhakikishia Naibu Waziri Mwakibete kuwa mradi huo utaendelea kutekelezwa na kukamilika kwa wakati.

 

Mradi wa upanuzi wa Bandari ya Ujiji ni sehemu ya Mradi Mkubwa unaohusisha maboresho ya Bandari hiyo, Bandari ya Kibirizi na Bandari ya Kigoma Mjini.