Habari
ULEGA AKOSHWA NA MIRADI 81 YA DHARURA
Waziri wa Ujenzi, Abdallah Ulega, ameonesha kuridhishwa kwake na kazi kubwa iliyofanywa na Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS), akiupongeza kwa usimamizi thabiti wa miradi 81 ya dharura iliyotekelezwa kote nchini.
Miradi hiyo, iliyohusisha ujenzi wa madaraja na makalvati kupitia mpango maalum wa CERC, imeelezwa kuwa mfano wa mafanikio ya kitaifa katika kukabiliana na changamoto za miundombinu hususan nyakati za mvua na mafuriko.
Akizungumza mkoani Morogoro wakati akifungua Mkutano wa 21 wa Baraza la Wafanyakazi wa TANROADS, Ulega amesisitiza kuwa miradi hiyo si tu imekamilika kwa wakati, bali pia imejengwa kwa viwango vya juu vya ubora na Makandarasi wazawa jambo linaloonesha kukua kwa uwezo wa ndani wa kitaalamu.
Waziri Ulega amemshukuru Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuridhia upatikanaji wa fedha za utekelezaji wa miradi hiyo, akibainisha kuwa uwekezaji huo umeanza kuzaa matunda.
Ameongeza kuwa licha ya mvua zinazoendelea kunyesha nchini mwaka huu, athari zake zimepungua kwa kiasi kikubwa ukilinganisha na miaka ya nyuma hali inayochangiwa na ubora wa miundombinu iliyojengwa.
“Miradi hii ya dharura ni alama ya uwezo wa wataalam wetu wa TANROADS katika kusimamia na kutekeleza kazi kwa umahiri mkubwa. Ni mfano hai wa namna tunavyoweza kukabiliana na changamoto za mafuriko nchini”, amesisitiza Ulega, huku akihimiza kuendelea kufanyika tathmini ya kina ili kubaini maeneo mengine yanayohitaji madaraja ya kisasa kama hayo.
