Tanzania emblem
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Wizara ya Ujenzi

Habari

TBA KUTUMIA MFUMO WA KIELETRONIKI KUFUATILIA MAKUSANYO YA KODI


Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu imeupongeza Wakala wa Majengo Tanzania (TBA) kwa kutumia mfumo wa kieletroniki kufuatilia makusanyo ya kodi za wapangaji katika majengo yao.

Akizungumza mara baaada ya kupokea Taarifa ya kiutendaji ya wakala huo, leo Tarehe 19 Oktoba, 2023 Bungeni, jijini Dodoma, Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Mheshimiwa Selemani Kakoso, amesema suala la ufuatiliaji wa kodi kwa njia ya kieletroniki utaleta mapato mengi kwa serikali.

“Tunawapongeza kwa kutumia mfumo huu wa kieletroniki, kwani mfumo huu umeleta mabadiliko makubwa, husasani katika kuongeza mapato kwa wakala”, amesema Mheshimiwa Kakoso.

Aidha, Mhe Kakoso ameishauri Wizara ya Ujenzi kuwaongezea bajeti Wakala huo ili kuwasaidia kukamilisha miradi yao na kufikia malengo waliojiwekea.

Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Ujenzi, Eng. Godfrey Kasekenya ameishukuru Kamati ya Bunge ya Miundombinu kwa kuendelea kupigania na kusimamia miradi mingi ya Wakala wa Majengo Tanzania (TBA), kwamba inafahamika na kupelekea kupata kazi ya ukarabati wa Uwanja wa Benjamini Mkapa.

Pamoja na hayo, Naibu Waziri Kasekenya ameongeza kwa kusema kuwa wakala huo unazidi kufanya vizuri katika kujenga majengo  mazuri yenye ubora wa kisasa Zaidi.

Naye,  Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Majengo Tanzani (TBA), Arch. Daud Kondoro, amesema kuwa kupitia Wizara na Sekta Binafsi Taasisi hiyo imekuwa na maendeleo kwa kuwekeza kwenye miradi yao.

Pia ameongeza kwa kusema kuwa kutokana na mfumo wa teknolijia wanaotumia, umewawezesha kuwa na ufuatiliaji mzuri wa kujua mpangaji aliyekuwa kwenye nyumba ni mpangaji sahihi ambaye amepewa mkataba na wakala huo.

“Kumekuwa na changamoto ya wapangaji kupangisha watu  ambao hawana mkataba katika nyumba zinazosimamiwa na Wakala huu, sisi kama TBA tunatumia mfumo wa kieletroniki pamoja na coart broker kufuatilia kila mpangaji kujua kama ni mpangaji halali ambaye amepewa mkataba na TBA”, amesema Arch. Kandoro

Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu leo imepokea Taarifa ya Utendaji wa TBA kwa kipindi cha Julai - Oktoba 2023 iliyowasilishwa na Naibu Waziri wa Ujenzi Eng. Godfrey Kasekenya kwa niaba ya Waziri wa Wizara hiyo Mheshimiwa Innocent Bashungwa.