Habari
TANZANIA NA DRC ZAJA KIVINGINE

Serikali za Tanzania na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo DRC kwa pamoja zimeingia makubaliano ya kuboresha miundombinu ya Barabara, Reli na Bandari ili kuongeza ufanisi katika biashara na hivyo kukuza uchumi wa nchi hizo.
Hafla ya makubaliano hayo imefanyika jijini Dar es Salaam ambapo Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi wa Tanzania, Prof. Makame Mbarawa amesema makubaliano yataimarisha miundombinu ya Reli, Barabara, Bandari na ujenzi wa Meli za mizigo na abiria.
"Tunakusudia kuongeza ufanisi wa kibiashara katika nchi zetu na hivyo kuimarisha uhusiano wa kindugu na kukuza uchumi wa nchi zetu", amesisitiza Prof. Mbarawa.
Prof. Mbarawa amesema miradi hiyo ambayo ujenzi wake utatekelezwa kwa awamu utapunguza muda wa safari kutoka DSM kwenda Lubumbashi nchini DRC na hivyo kupunguza gharama za biashara na muda wa kusafirisha mizigo toka siku 30 hadi wiki moja.
Waziri wa Miundombinu wa DRC, Alexis Mavunyi amesema namna mataifa hayo mawili yatakavyo nufaika kutachochea uzalishaji wa bidhaa, mazao na biashara zingine hivyo kukuza uchumi wa nchi hizo na raia wao.
Kwa upande wake, Mtendaji Mkuu wa Taasisi ya Ushoroba wa Kati, Wakili Froly Okanju amesema makubaliano hayo yatafungua fursa kubwa ya usafirishaji kwa nchi za ushoroba wa kati ambazo zinakwenda kupata maendeleo kwa kuwa zinaitegemea Tanzania katika uingizaji wa mizigo na hivyo kuitaka Tanzania kujipanga kuhudumia nchi za ushoroba huo kikamilifu.
Pamoja na mambo mengine ujenzi wa Miradi hiyo inayotarajiwa kuanza utekelezaji wake baadae mwakani itatoa fursa kwa Serikali za Tanzania, DRC, Wadau wa Maendeleo ya kuzalisha nafasi za ajira.
Viongozi hao pamoja na ujumbe wao wametembelea Shirika la Reli TRC na Mamlaka ya Bandari nchini TPA na kufurahishwa na namna taasisi hizo zinavyofanya kazi kwa weledi na ubunifu.