Tanzania emblem
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Wizara ya Ujenzi

Habari

TANROADS HAKIKISHENI MAWASILIANO YANAREJEA BARABARA ZOTE DAR-KASEKENYA


NAIBU Waziri wa Ujenzi, Mhandisi, Godfrey Kasekenya ameuagiza Wakala wa Barabara Nchini (TANROADS) kufanya kazi usiku na mchana ili kurejesha mawasiliano ya miundombinu ya Barabara na madaraja yalioathiriwa na mvua kubwa iliyonyesha juzi jijini Dar es salaam.

Waziri Kasekenya ameyasema hayo leo jijini Dar es salaam wakati akikagua miundombinu ya madaraja na Barabara zilizoathiriwa na mvua katika wilaya za Ilala na Kinondoni ambapo ameipongeza TANROADS kwa kufanikiwa kurudisha mawasiliano ya barabara ya Mbuyuni Kunduchi hadi Ununio ambayo ilikuwa haipitiki.

Waziri Kasekenya amesema Serikali imejipanga ipasavyo kukabiliana na changamoto zitakazosababishwa na mvua zinazoendelea kunyesha nchini na kuwataka wananchi kutoa ushirikianao kwa TANROADS ili kuepuka madhara katika msimu huu wa mvua.

"TANROADS hakikisheni kwamba daraja hili linamazika kupitika pande zote mbili na kuweka kingo imara na alama elekezi ili kuwawezesha wananchi kutumia daraja hili usiku na mchana,” amesema Kasekenya.

Amewaonya wananchi kuacha kuharibu mazingira jirani na mito, kuacha kuchimba mchanga na kutupa taka ovyo hali inayodhoofisha kingo za mito na kurahisisha mafuriko.

Naye Mkuu wa Kitengo cha Matengenezo cha Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) mkoa wa Dar es salaam, Mhandisi,  Suzana Lucas amesema kwamba mvua zilizoanza kunyesha jijini Dar es salaam zimesababisha athari za miundombinu ya Barabara na madaraja yakiwemo lakini kazi ya kuiboresha miundombinu hiyo ili ipitike inaendelea na itakamilika katika muda mfupi ujao.

Ameyataja madaraja yalioothirika kuwa ni pamoja na daraja la Mtongani Kunduchi, daraja la Mpiji na daraja la Tegeta ambapo amemhakikishia naibu waziri kasekenya kuwa kazi zitafanyika usiku na mchna hadi zikamilike.

"TANROADS Dar es salaam na makao makuu  tumefanya kazi usiku na mchana kuhakikisha mawasiliano yanarejea na hivi sasa daraja linapitika na shughuli zinaendelea," amessisitiza Eng. Suzana.

Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni, Mhe. Saad Mtambule ameshukuru Serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Raisi Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa jitihada kubwa walizofanya na kurudisha mawasiliano kwa haraka.

Vile vile amewapongeza TANROADS na TARURA kwa kushirikiana na kufanya kazi usiku na mchana kwenye daraja la Mpjiji na Kunduchi Mtongani na kurejesha huduma ya usafiri kwa wananchi,

Mwisho ametoa wito kwa wananchi kuchukua tahadhari wakati wa mvua na kuwataka  kusafisha mifereji na kuepuka shughuli za uharibifu wa mazingira katika mito inayopitisha maji ya mvua ili kulinda madaraja na barabara na hivyo kuepusha athari kwa wananchi.

Naibu waziri kasekenya anaendelea na ziara yake mkoani Dar es salaam kukagua na kutoa ufumbuzi kwa changamoto zilizosababishwa na mafuriko yaliotokea mwishioni mwa wiki na kuathiri barabara na madaraja kadhaa katika wilaya ya Kinondoni na Ilala.