Tanzania emblem
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Wizara ya Ujenzi

Habari

PROFESA MBARAWA ASISITIZA USHIRIKIANO WIZARA MPYA


Waziri wa Uchukuzi, Prof. Makame mbarawa  ametoa wito kwa menejimenti ya Wizara kushirikiana na wakuu wa taasisi  kuhakikisha kunakuwa na usimamizi madhubuti na wenye tija kwenye miradi inayoendelea ili iweze kukamilika kwa wakati na kwa thamani halisi ya fedha.

Prof. Mbarawa ameyasema hayo leo jijini Dodoma, mara baada ya kuwasili katika Wizara mpya, na kuwataka watumishi wa Wizara hiyo,kuwa na ushirikiano baina yao na kuongeza ufanisi wa kazi.

Aidha, Waziri Mbarawa, amesema kuwa Wizara ya Uchukuzi, ni moja ya Wizara ambayo ina miradi mingi na mikubwa ambayo ongeza tija kwenye maeneo ya usimamizi na uendeshaji pamoja na uboreshaji wa miundombinu.

“awali ya yote napenda kumshukuru Mhe Rais wa awamu ya sita Dkt Samia Suluhu Hassan kwa kuniamini tena na kuniteua kumsaidia tena,  na sasa ni katika Wizara ya Uchukuzi, ni wizara ambayo ina miradi mingi ya kimkakati kwa ajili ya maendeleo ya Nchi yetu ikiwemo Ujenzi wa Reli ya kisasa ya SGR, uboreshaji wa bandari  na ununuzi wa ndege hivyo tufanye kazi ya kuleta matokeo kwa manufaa ya wananchi na Taifa kwa ujumla” amesema Prof Mbarawa

Kwa upande wake Naibu Waziri wa U chukuzi Mhe David  Kihenzile amesema ili Wizara ifikie malengo yaliyokusudiwa ni vyema viongozi pamoja na watumishi wote wa Wizara wakafanya kazi kama timu moja na kuongeza kuwa watendaji wa Wizara na Taasisi zake zote sasa wanapaswa kubadili fikra.

“Nawapongeza watumishi wote wa Wizara kwa mapokezi  mazuri na namshukuru Mhe Rais Dkt Samia Suluhu Hassan kwa kuwa na imani na mimi na kuniteua kumsaidia katika wizara hii ya Uchukuzi kama Naibu Waziri, tuendelee kufanya kazi kwa pamoja  na kwa ushirikiano” amesema Mhe Kihenzile

Naye Katibu Mkuu wa Wizara ya Uchukuzi, Prof. Godius  Kahyarara amesisitiza kutoa ushirikiano mzuri  na Wizara hiyo na kuwataka watumishi kutekeleza majukumu yao kwa wakati na ufanisi.