Tanzania emblem
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Wizara ya Ujenzi

Habari

NDUHIYE AWATAKA WANAWAKE WATAALAM WA UJENZI KUCHANGAMKIA FURSA


Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi (Sekta ya Ujenzi), Bw. Ludovick Nduhiye amesema Serikali itaendelea kushirikiana na taasisi mbalimbali zenye lengo la kuwajengea uwezo wakadiriaji majenzi, wasanifu majengo na wahandisi wanawake ili kuwa nasifa za kuajiriwa, kujiajiri na kuajiri wengine.

Akizungumza katika hafla ya ufunguzi wa Programu ya kuwawezesha wanawake katika masuala ya ujenzi iliyoandaliwa na taasisi ya wasanifu majengo Tanzania, (TAWAH) jijini Dar es Salaam amezungumzia umuhimu wataalam hao kufanya mazoezi ya vitendo kwa wingi ili kuwa na ujuzi na hivyo kuwawezesha wanawake kushiriki katika maendeleo ya sekta ya ujenzi nchini.

"...Serikali inatenga asilimia 30 ya Bajeti ya Ujenzi wa Barabara kwa ajili ya miradi inayotekelezwa na wanawake hivyo waongezeeni ujuzi ili waweze kunufaika na fursa hiyo," amesema Naibu Katibu Mkuu Nduhiye.

 

Nduhiye amezungumzia umuhimu wa wataalam wa ujenzi wanawake kuunda vikundi kufungua kamapuni na kuoba kazi za ujenzi na Serikali itawaunga mkono katika hatua zote.

Kwa upande wake, Mdhibiti ubora wa Bidhaa za Kampuni ya Saruji ya Tanga, Bw. Shukrani Chindoli amewataka waalam wa ujenzi kuzingatia usalama wakati wote ili kufanya sekta ya uje kuwa mahali salama pa watu kufana kazi.

Naye Msajili wa Bodi ya Wasanifu Majengo na Wakadiriaji Majenzi Arch. Edwin Nunduma ameipongeza TAWAH kwa jitihada inazofanya kuwawezesha wataalam wa ujenzi wanawake na kuahidi kushirikiana nayo ili wataalam hao wasajiliwe na kuwa na sifa za kufanya kazi ndani na nje.

Mwenyekiti wa Taasisi ya Wanawake Wasanifu Majengo Tanzania (TAWAH), Arch. Siti Sheuya ameishukuru Serikali kwa jitihada inazozifanya kuwawezesha wataalam wa ujenzi wanawake na kuahidi kuwa watazingatia uzalend, uadilifu na kufanya kazi kwa bidiii.