Tanzania emblem
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Wizara ya Ujenzi

Habari

KAMATI YA MIUNDOMBINU YASHAURI TBA UJENZI WA NYUMBA ZA KISASA


Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu imeutaka Wakala wa Majengo Tanzania (TBA) kuhakikisha inajenga nyumba za kisasa ambazo zinaendana na uhalisia ili kukidhi mahitaji ya washitiri wake.

Hayo yamesemwa jijini Dodoma na Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Mheshimiwa Suleiman Kakoso, mara baada ya Kamati hiyo kupokea taarifa ya utendaji kazi wa Wakala huo pamoja na Wakala wa Ufundi na Umeme (TEMESA).

Mheshimiwa Kakoso, amesema kuwa sambamba na hilo Wakala huo umetakiwa kuhakikisha unaongeza ubunifu katika utekelezaji wa miradi yake ili kuweza kukidhi soko la ushindani nchini na nje ya nchi.

“Kamati imeridhishwa na utekelezaji wa miradi yenu, ila hakikisheni mnaweka mikakati inayotekelezeka kwani uwekezaji kwenye ujenzi wa nyumba unakuwa na kubadilika kila siku hivyo mnatakiwa mwende sambamba na mabadiliko hayo ili kuweza kupata wateja ndani na nje ya nchi”, amesema Kakoso.

Aidha, Kakoso ameutaka Wakala huo pia kuhakikisha wanaendeleza na kubuni miradi mbalimbali katika maeneo ambayo wanamiliki ili kulinda maeneo yao pamoja na kusambaza huduma maeneo mbalimbali nchini.

Kuhusu utendaji wa kazi wa TEMESA, Kamati imeishauri Wizara kuusimamia kwa karibu Wakala huo ili kuweza kuleta tija na kupunguza na changamoto ambazo zinaukabili.

Kwa upande wake, Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, Profesa Makame Mbarawa, amesisitiza TBA kuendelea kuwa wabunifu kwa kuhakikisha unaendelea kujenga na kukarabati nyumba na majengo ya Serikali ili kuongeza ubora wa makazi kwa viongozi na watumishi wa umma.

Waziri Mbarawa ametaja miradi ya kitaifa mikubwa ambayo imetekelezwa na TBA kuwa ni ujenzi wa nyumba za makazi za Magomeni Kota, jengo la Mama na Mtoto katika Hospitali ya SekouToure Mwanza, jengo la Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Ujenzi wa makazi ya Rais Mstaafu wa Awamu ya Nne na Usimamizi wa mradi wa ujenzi wa Ikulu Chamwino Dodoma.

Kuhusu Wakala wa Ufundi na Umeme (TEMESA) Waziri Mbarawa ameushauri Wakala huo kuendelea kushirikisha Sekta Binafsi katika uendelezaji wa karakana zao kama walivyofanya kwenye vivuko kwa kuruhusu Kampuni ya Azam Marine kutoa huduma za usafirishaji kati ya Magogoni na Kigamboni jijini Dar es salaam na hivyo kupunguza malalamiko ya wateja.

Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu, imepokea, kujadili na kushauri taarifa ya Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi kuhusu masuala mbalimbali ya kiutendaji ya Wakala wa Majengo Tanzania (TBA na Wakala wa Ufundi na Umeme (TEMESA).