Habari
KADCO WATAKIWA KUHAMASISHA UTALII.

Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, Profesa Makame Mbarawa ameitaka Kampuni ya Uendelezaji Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Kilimanjaro (KADCO) kuhakikisha inahamasisha mashirika mengi zaidi ya Ndege kutumia kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Kilimanjaro (KIA) kutimiza ya dhamira ya Serikali ya kuitangaza utalii.
Akizungumza mkoani Kilimanjaro katika uzinduzi wa safari ya kwanza ya Shirika la Ndege za Eurowings kutokea nchini Ujerumani kuja Tanzania kupitia Kiwanja cha KiA, Prof. Mbarawa amesema kuanza kwa safari za shirika hilo nchini ni miongoni mwa matokeo ya filamu ya Royal Tour iliyofanywa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan.
“Hakikisheni mnashawishi mashirika mengi zaidi ya ndani na nje kutumia kiwanja hiki, ili kuutangaza utaliii na matokeo ya safari hizo yataongeza pato la Taifa na ajira kwa Watanzania” amesema Waziri Prof. Mbarawa.
Mbarawa ameitaka KADCO kuboresha mahusiano na makampuni ambayo yanatumia kiwanja hicho ili kuhamasisha kampuni zilizopo na kuhamasisha kampuni mpya ili kuongeza idadi ya safari kwa kiwanja hicho ambacho kinapokea watalii wengi nchini.
“Lazima muhakikishe mashirika yaliyoanza kutoa huduma hayasitishi safari zake kwani kwa kufanya hivyo tutaongeza uaminifu kwa wateja wetu ambao ni mashirika ya ndege lakini pia hatutatumia nguvu nyingi kuvutia mashirika mengine kuleta abiria nchini", amefafanua Waziri Prof. Mbarawa.
Kwa upande wake Balozi wa Ujerumani Nchini, Regina Hess, amesema Serikali ya nchi hiyo itaendeleza mahusiano mazuri yaliyopo kati yake na Tanzania na itaendelea kuleta watalii wengi zaidi nchini ili kuja kuona vivutio mbalimbali vilivyopo.
Naye Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Stephen Kigaigai amesema mkoa umejipanga vizuri kuhakikisha wageni wote wanaotumia kiwanja hicho wanapewa huduma na ukarimu ili kuwafanya kuitangaza nchi wanaporudi nchini kwao.
Mwenyekiti wa Bodi ya KADCO, Dkt. Natu Mwamba, amesema KADCO itaendelea mahusiano mazuri na makampuni ya ndani nan je yanayotumia kiwanja hicho na kusisitiza kuwa inaendelea kujitangaza zaidi ndani nan je ya nchi ili kuvutia mashirika mengi zaidi ili kuendelea kuitangaza nchi zaidi.
Kampuni ya Eurowings imeanzisha rasmi safari zake nchini ambapo itakuwa na safari nne kwa wiki, safari mbili zitakuwa kutoka Nchini Ujerumani kupitia kupitia Mombasa na KIA na mbili zitakuwa kutokea nchini Ujerumani kwenda Kisiwani Zanzibar.