Tanzania emblem
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Wizara ya Ujenzi

Habari

DARAJA LA J.P MAGUFULI LIMEFIKIA 78%, MKANDARASI ANALIPWA KWA WAKATI: BASHUNGWA


Waziri wa Ujenzi, Innocent Bashungwa amesema kuwa serikali inalipa kwa wakati madai yote yanayowasilishwa na Mkandarasi anayetekeleza ujenzi wa daraja la J.P Magufuli (Kigongo – Busisi) lenye urefu wa kilomita 3.0 na Barabara unganishi zenye jumla ya kilometa 1.66 lililopo jijini Mwanza ambapo ujenzi umefikia asilimia 78 ya Utekelezaji.
Ameyasema hayo Oktoba 11, 2023 akiwa Mwanza katika ziara ya kukagua Daraja hilo linalounganisha Barabara Kuu ya Usagara - Sengerema - Geita katika Ziwa Victoria kwa kugharimiwa na Serikali kwa jumla ya shilingi Bilioni 716.3

Bashungwa amesema kuwa Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan Ujenzi wa Daraja hilo ameupa kipaumbele kikubwa kwa kuhakikisha Mkandarasi hatoki nje ya mradi kwa kutoa fedha kuwezesha madai yote ya mkandarasi kulipwa ndani ya muda ili kuhakikisha anafanya kazi bila kusimama.

“Mheshimiwa Rais anaendelea kuonesha kwa vitendo kaulimbiu yake ya awamu ya sita ya kazi iendelee ambayo inamaanisha kijiti ambacho alikipokea kutoka kwa kaka yake Hayati Dkt. John Pombe Magufuli ameendeleza pale alipoishia ikiwemo mradi huu wa historia kwa nchi yetu”, amesema Bashungwa.

Aidha, Bashungwa ameeleza kuwa Mheshimiwa Rais anahakikisha hakuna madai yanayowasilishwa na mkandarasi huyo ambayo hayalipwi na amemuomba Mkuu wa Mkua wa Mwanza, Amos Makalla, kupita mara kwa mara katika mradi huo ili kuhakikisha kazi inaendelea kwa sababu mkandarasi  hana sababu yeyote ya kutoendelea na kazi kwani malipo yote yanafanyika kwa wakati.

Amemshukuru Mheshimiwa Rais kwa kuendelea kuifungua Mikoa ya kanda ya ziwa ambapo kwa muunganiko wa Bandari pamoja na mradi wa Reli ya kisasa ya SGR,  mizigo kutoka nchi mbali mbali duniani itatumia miundombinu hiyo kusafirisha mizigo yao na hivyo kunufaisha ukanda huu wa ziwa kwa kupitia kituo kikubwa cha SGR cha Misungwi.
 

“Tunaposema Kazi Iendelee ni kama hivi miradi yote inayotumia mabilioni ya fedha inatekelezwa hivyo nawaomba watanzania tuendelee kuwa wamoja kwani mradi huu utafungua fursa za kiuchumi kwa wananchi wa kanda ya ziwa na mikoa ya jirani” ameongeza Bashungwa.

Awali akitoa taarifa ya daraja hilo, Mkurugenzi wa Miradi kutoka Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) Eng Boniface Mkumbo amesema kuwa hadi sasa mkandarasi ameshalipwa jumla ya shilingi bilioni 396.3 ambazo zinajumuisha malipo ya awali pamoja na hati zote za madai 17 alizowasilisha hivyo hadai malipo yoyote.

Amesema kuwa lengo la ujenzi wa daraja hilo ni kuunganisha barabara kuu ya Usagara – Kisesa – Geita yenye urefu wa kilomita 90 katika ushoroba wa ziwa Victoria ambayo inaanzia Sirari mpakani mwa Tanzania na Kenya hadi Mutukula mpakani mwa Tanzania na Uganda (km 774)

Mkumbo amesema kuwa kwa sasa barabara hii inaunganishwa kwa kutumia vivuko vikubwa vitatu na kutokana na idadi kubwa ya magari yanayopita kwa siku huweza kutumia masaa mawili hadi matatu kuvusha magari kutoka upande mmoja hadi mwingine.