Tanzania emblem
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Wizara ya Ujenzi

Habari

BILION 45 KUTUMIKA UJENZI WA BARABARA YA NTENDO - MUZE


Serikali inatarajia kutumia takribani Shilingi Bilioni 45 kwa ajili ya ujenzi wa barabara ya Ntendo hadi Muze yenye urefu wa kilomita 25 kwa kiwango cha lami ili kurahisisha shughuli za usafiri na usafirishaji.

 Hayo yamesemwa mkoani Rukwa na Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi Prof. Makame Mbarawa, wakati akikagua mradi huo ulioanza kutekelezwa na unatarajiwa kutumia muda wa miezi 18 ambapo pamoja na mambo mengine ameeleza kuwa uzalishaji wa mazao unakwenda sanjari na uboreshaji wa miundombinu ili kurahisisha bei na ufikaji wa haraka wa mazao kwa wateja.

 “Mkoa huu unazalisha mazao mengi sana ambayo yanahitaji kufika kwa wakati kutoka eneo moja hadi jingine hivyo Serikali imeanza kujenga barabara hii kwa kilomita 25 lengo ni kuhakikisha gharama za usafirishaji zinapungua kupitia miundombinu wezeshi” amesisitiza Waziri Mbarawa.

Waziri Prof. Mbarawa ameutaka Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) kuhakikisha inamsimamia kwa karibu Mkandarasi anayejenga barabara hiyo kutoka kampuni ya China Geo Engineering Corporation ili ikamilike kwa viwango na kwa wakati.

 Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya wa Sumbawanga,  Sebastiani Waryuba,  ameahidi kutoa ushirikiano kwa Mkandarasi ili kuuwezesha mradi huo kukamilika na kuahidi kukamilisha taratibu za fidia kwa wale wananchi wanaodai na  watalipwa kulingana na viwango vilivyowekwa kisheria.

 Mkuu wa Wilaya huyo ameipongeza Serikali kwa kuendelea kuboresha miundombinu katika mkoa huo hali itakayorahisisha usafirishaji, kupunguza gharama na kuongeza pato kwa wananchi wa mkoa huo kupitia usafirishaji wa mazao.

 Kwa upande wake Kaimu Meneja wa TANROADS Mkoa wa Rukwa, Eng.  Nyamweru Fashe, amesema mpaka sasa mradi umefikia asilimia sita na kwa sasa Mkandarasi anaendelea na kazi ya kukamilisha matabaka mbalimbali ya awali ya barabara.

 Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi Prof. Makame Mbarawa yuko Mkoani Rukwa kwa ziara ya siku moja ya kukagua miradi mbalimbali ya maendeleo inayotekelezwa na Wizara.