Tanzania emblem
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Wizara ya Ujenzi

Habari

BASHUNGWA AMVAA MKANDARASI BARABARA YA MZUNGUKOWA NJE YA DODOMA


Waziri wa Ujenzi, Innocent Bashungwa amemuagiza Mkandarasi Avic anayejenga barabara ya mzunguko wa nje ya Dodoma, yenye urefu wa Kilometa 112.3 sehemu ya Ihumwa Dry Port - Matumbulu - Nala (km 60), kuhakikisha anakamilisha barabara hiyo ifikapo mwezi Desemba, 2024.

Bashungwa ametoa agizo hilo Septemba 29, 2023, jijini Dodoma wakati akikagua maendeleo ya ujenzi wa barabara hiyo ambapo pamoja na mambo mengine amemsisitiza mkandarasi huyo kuongeza spidi kwenye ujenzi wa madaraja mawili ambayo yanaonekana kuchelewa ujenzi wake.

“Sipepesi macho kwenye usimamizi wa mikataba, kufanya kazi kwa ubora na kasi ndio kipimo chako, ukizembea kwenye kazi hii usahau kupewa kazi nyingine za ujenzi kwenye Sekta hii nchini”, amesema Bashungwa.

Ameahidi kutembelea tena mradi huo ifikapo Desemba mwaka huu ili kuona uetekelezaji wa maagizo yake na kumsisitiza Mkandarasi huyo kufanya kazi usiku na mchana ili uweze kukamilika kwa wakati kulingana na maelekezo ya Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Aidha, Bashungwa ameuagiza Wakala ya Barabara Tanzania (TANROADS), kushirikiana na Shirika la Reli (TRC), kurudisha haraka mawasiliano ya barabara ya lami eneo la Mkonze na Nala ambalo lilibomolewa kwa ajili ya ujenzi wa reli ya SGR kwani wananchi wamekuwa wakipata kero kutokana na changamoto katika maeneo hayo.

Bashungwa amewataka wakandarasi nchini wanaotekeleza miradi ya ujenzi kuhakikisha wanatekeleza miradi hiyo kwa mujibu wa Mkataba na kusisitiza kutokuwa na huruma kwa yeyote atakayekiuka mikataba hiyo.

Bashungwa amemuagiza Mhandisi Mshauri Mzawa wa kampuni ya Inter-Consult kumsimamia mkandarasi wa kampuni ya China Civil Engineering Corporation (CCEC) anayetekeleza sehemu ya Nala - Veyula - Mtumba (km 52.3), kutoa vifaa vya usalama kwa wafanyakazi wake ili kuepukana na madhara yanayoweza kutokea maeneo ya kazi.

Katika hatua nyingine, Bashungwa amewaagiza Mameneja wa TANROADS wa mikoa yote nchini kuhakikisha wanazibua mifereji ya barabara zilizo chini ya Wakala huo kabla ya mvua hazijaanza ili zisiwe chanzo cha kuleta mafuriko, sambamba na hilo Waziri huyo amempongeza Meneja wa TANRODS Mkoa wa Dar es Salaam kwa kufanya matengenezo na kuzibua barabara na mifereji katika mkoa huo.

Kwa upande wake, Mtendaji Mkuu wa TANROADS, Eng. Mohamed Besta ameeleza kuwa mpaka sasa sehemu ya mradi kutoka Nala – Veyula – Mtumba (km 52.3) umefika asilimia 54.3 na sehemu inayoanzia Ihumwa Dry Port – Matumbulu – Nala umefika asilimia 50 na sasa wakandarasi wanaendelea na kazi mbalimbali za ujenzi wa makalavati na madaraja makubwa mawili.

Mradi wa Barabara ya Mzunguko wa nje ya Dodoma (Km 112.3), unagharimiwa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kushirikiana na Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB) kwa gharama ya shilingi Bilioni 221 na unatarajiwa kukamilika mwezi Desemba 2024.