Tanzania emblem
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Wizara ya Ujenzi

Habari

Barabara ya Same – Mkomazi kujengwa kwa lami.


Naibu Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi Eng. Godfrey Kasekenya amesema Serikali iko katika hatua za mwisho za maandalizi ya ujenzi wa barabara ya Same - Kisiwani-Mkomazi yenye urefu wa (KM 96.46).

Akikagua maandalizi ya ujenzi wa barabara hiyo Eng. Kasekenya amesema awamu ya kwanza ya ujenzi huo itahusisha KM 11.9 ambapo ujenzi utaanzia sehemu ya Mroyo - Ndungu hadi Kihurio.

Barabara hiyo ambayo inapita pembezoni mwa hifadhi ya taifa ya Mkomazi itachochea na  kurahisisha huduma za usafiri na uchukuzi, kilimo, utalii na biashara kwa wakazi wa tarafa za Gonja, Ndungu, Kihurio, Bendera na Mkomazi wilayani Same na hivyo kukuza uchumi wa wakazi hao.

 “Tumejipanga kuijenga barabara hii kwa lami na kuhakikisha inakamilika kwa wakati na ubora uliokusudiwa”, amesisitiza Naibu Waziri Kasekenya.

Aidha amekagua ujenzi wa madaraja ya Mamba na Yongoma ambayo ujenzi wake umekamilika katika barabara ya Mwembe-Myamba-Ndungu na kuzungumzia umuhimu wa wananchi kulinda miundombinu hiyo ili itumike wakati wote wa mwaka.

Naye Meneja wa Wakala wa Barabara (TANROADS), Mkoa wa Kilimanjaro Eng. Motta Kyando amesema ujenzi wa madaraja na makalvati katika barabara ya Mwembe hadi Ndungu ni zoezi endelevu hivyo kuwataka wananchi kuepuka kulima karibu na hifadhi ya barabara ili kuepuka mmomonyoko wa udongo.

Naye Mbunge wa Same Mashariki Mhe. Anne Kilango Malechela amesema ujenzi wa barabara ya Same-Kisiwani-Mkomazi (KM 96.46), na Mwembe-Myamba-Ndungu (KM 90.19), ukikamilika utafungua uchumi wa wakazi wa wilaya ya Same ambao kwa kiasi kikubwa unategemea shughuli za kilimo cha mazao ya tangawizi na ndizi na kuhuisha  utalii katika hifadhi ya taifa ya Mkomazi.