Tanzania emblem
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Wizara ya Ujenzi

Habari

BANDARI KAVU YA KWALA MAMBO YAMEIVA.


Naibu katibu Mkuu Sekta ya Uchukuz, Dkt Ally Possi amezitaka taasisi za  Mamlaka ya Usimamizi wa  Bandari Tanzania (TPA), Shirika la Reli (TRC) na  Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) kuhakikisha  wanaweka Mazingira Rafiki kwa wafanyabiashara ili  kuanza kutumia Bandari kavu ya kwala kwani kwasasa ujenzi wa Bandari hiyo umefikia asilimia 98.

Possi ameyasema hayo kwenye kikao kilichowakutanisha wafanyabishara wa Bandari, Wizara, TRC na TRA, katika kuboresha  utendaji kazi wa bandari ya Dar es Salaam.

“Ujenzi wa Bandari Kavu ya Kwala umefikia asilimia 98 hivyo taasisi zote zinatakiwa ziwezeshwe kuhamia ili kupunguza Msongamano wa  Mizigo katika  Bandari ya Dar es Salaam” alisema Dkt.Possi

Aidha, Dkt. Possi amezielekeza taasisi hizo kutoongeza gharama katika kusafirisha Mizigo kutoka Bandari ya Dar es Saalam Mpaka kwala, kwani kuongezeka kwa gharama kutaongeza wafanyabiashara kutotumia bandari hiyo.

Baadhi ya wafanyabiashara katika sekta ya Bandari wamesema kuwa wapo tayari kutumia Bandari ya Kwala  kwani bandari hiyo itasaidia kupunguza Mizigo katika Bandari ya  Dar es Salaam, hivyo wanaomba Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi  (Sekta ya Uchukuzi), kuendelea kusimaia  mifumo ya utoaji huduma  ili kusiwe na usumbufu.

Naye Meneja Uendeshaji kutoka Shirika la Reli Tanzania (TRC) Focus Sahani amesema tayari Shirika hilo limeshatenga Mabehewa pamoja  na  vichwa vya treni kwa ajili ya kuanza kusafirisha Mizigo kutoka Bandari ya Dar es Salaam  kwenda Kwala.

Kwa upande wake Meneja Msimamizi wa Ujenzi wa Bandari hiyo Alexander  Ndibalema amesema kuwa ujenzi  wa miundombinu ya reli na Barabara ya Kilometa 15 kutoka Vigwaza mpaka Kwala umekamika hivyo Bandari  hiyo ipo   tayari kuanza kazi.